Kocha mpya aliyeteuliwa juzi Manuel Preciado amefariki saa 24 baada ya kutangazwa kama Kocha wa klabu ya Uhispania, Villarreal. Kocha huyo ambaye hapo zamani alikua kocha wa Sporting Gijon alifariki kutokana na mshtuko wa moyo akiwa na umri wa miaka 54. Kifo chake kimetokea saa 24 baada ya kukubali mkataba wa kuiongoza klabu ya Villareal iliyoshuka daraja, ambapo mkataba wake ulikua wa kuanza msimu wa mwaka 2012 hadi 2013. Preciado alifutwa kazi na Sporting Gijon mnamo mwezi Januari licha ya kuiwezesha klabu hio kupanda daraja mara mbili kuingia Ligi kuu ya Uhispania, La Liga. Mnamo mwezi Aprili mwaka 2011, klabu yake ya Sporting Gijon iliikwamisha klabu maarufu ya Real Madrid kwa kuvunja rekodi yake ya miaka tisa bila kupoteza kwenye uwanja wa nyumbani safari hii ikiwa chini ya Jose Mourinho. Wakati wake wa uchezaji soka Preciado alicheza kama beki aliyeanzia uchezaji wake katika klabu ya Racing Santander na pia kushiriki mechi za vilabu kama Linares, Mallorca, Alaves, Ourens...